Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) yenye makao yake mjini The
Hague Uholanzi imeitaka serikali ya Libya yenye makao yake Tripoli
imkabidhi kwa mahakama hiyo Saiful Islam Gaddafi mwana wa kiume wa
dikteta wa zamani wa Libya Kanali Muammar Gaddafi.
Saiful Islam Gaddafi
alikuwa amekatiwa hukumu ya kunyongwa na mahakama moja ya Tripoli. Bi
Fatou Bensouda Mwendesha Mashtaka Mkuu wa mahakama ya ICC amesema katika
ripoti aliyoiwasilisha kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa,
pamoja na kuwa mahakama hiyo ilishawaomba rasmi kwa mara kadhaa viongozi
wa Tripoli ili wamkabidhi Saiful Islam Gaddafi kwa mahakama ya jinai
ya ICC, lakini serikali ya Libya imekuwa ikipinga maombi hayo.
Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) mwaka 2011 ilitoa waranti wa
kutiwa mbaroni Saiful Islam Gaddafi kutokana na jinai dhidi ya binadamu
alizotenda huko Libya.
Mahakama ya Rufaa ya Tripoli mwishoni mwa mwezi
Julai mwaka jana iliwahukumu kunyongwa shakhsia kumi wa utawala wa
zamani wa Libya akiwemo mwana huyo wa Muammar Gaddafi baada ya
kupatikana na hatia ya kuwaua wafanya maandamano, kuasisi makundi ya
kukandamiza mapinduzi ya wananchi katika matukio ya Februari 17 Februari
mwaka 2011 na pia kuhusika katika ufisadi nchini.
No comments:
Post a Comment